Breaking

Ijumaa, 22 Mei 2020

Somo: Je Wajua Kama Mungu Anaweza Kubadilisha Maisha Yako Na Kukuinua ?


Mwalimu:  Apostle Daniel Stanslaus

Bwana Yesu asifiwe.Wanadamu wengi wameshindwa kufanikiwa kwa sababu ya historia ambazo zipo tayari katika familia zao.Historia hizi zimewafanya watu washindwe kuthubutu kufanya kitu fulani cha mafanikio pale fursa inapokuwa inatokea,Pale fursa inapotokea labda ya biashara, kazi ,Elimu au chochote kile cha mafanikio unakuta mtu kwa kuangalia historia ya familia yake kwamba hakuna mtu aliyewahi kufanya hicho kitu akafanikiwa ,hofu inamuingia na anasema kuwa sisi kwetu hatujawahi kufanya mambo kama hayo na kama tukifanya huwa hatufanikiwi.Kwa kufanya hivi watu wengi wamekosa Baraka ambazo Mungu alikuwa amewaandalia.Mungu huwa analeta fursa kwetu
kwa kuwa anatupenda na anatamani tutumie hizo fursa vizuri ili tufanikiwe na tuifanye kazi yake, kwa sababu ya kuangalia historia zetu tunajikuta tunabaki hivyo hivyo wala hatusogei mbele katika maisha yetu ya kila siku.

Mungu wetu sio mwanadamu, anao uwezo wa kubadilisha historia ya maisha yako na kukupandisha utukufu hadi utukufu kila iitwapo leo.Mungu anachotaka kwako ni Imani,umuangalie yeye na kamwe usiangalie ulipotoka au historia ya familia yenu inasemaje.Unaweza kutoka historia ya familia zinazoabudu miungu,familia za kilevi,familia zenye historia ya uzinzi,umasikini, lakini Mungu anaweza akakubadilisha wewe na kukufanya Mtumishi wa Mungu na kukupa utajiri ili watu kupitia wewe waone utukufu wa Mungu na Mungu mwenyewe ajitwalie Utukufu.Isaya 43:18-19(Msiyakumbuke mambo ya kwanza, wala msiyatafakari mambo ya zamani,Tazama, nitatenda neno jipya; sasa litachipuka; je! Hamtalijua sasa? Nitafanya njia hata jangwani, na mito ya maji nyikani.)Kupitia haya maandiko Mungu anatuambia kuwa tusiyakumbuke mambo ya zamani,yaani zile Historia zetu na historia za familia zetu kwa kuwa yeye Mungu atafanya jambo jipya katika maisha yetu tena atatengeneza njia hata pale pasipo na njia.Hata kama mazingira unayopitia ni magumu kwa namna gani Mungu amesema kuwa atabadilisha historia ya maisha yako na kukutengenezea njia ambayo itakupeleka kwenye mafanikio pasipo kuangalia historia yako.Mungu anataka utayari wako wa kusonga mbele pasipo kuangalia nyuma.

Waebrania 7:14-17(Maana ni dhahiri kwamba Bwana wetu alitoka katika Yuda, kabila ambayo Musa hakunena neno lo lote juu yake katika mambo ya ukuhani.Tena hayo tusemayo ni dhahiri sana zaidi, ikiwa ametokea kuhani mwingine mithili ya Melkizedeki;asiyekuwa kuhani kwa sheria ya amri iliyo ya jinsi ya mwili, bali kwa nguvu za uzima usio na ukomo;maana ameshuhudiwa kwamba, Wewe u kuhani milele Kwa mfano wa Melkizedeki.)
Katika Agano la kale makuhani walikuwa wakitoka katika kabila la Lawi.Ukisoma katika hayo maandiko utagundua Bwana Yesu hakutoka katika kabila la Lawi lakini alifanyika kuhani tena kuhani mkuu na mstari wa 16 unasema alifanyika sio kwa jinsi ya Mwili bali kwa Nguvu ya Uzima

KUMBUKA HAYA YAFUATAYO
:
Mungu anao uwezo mkubwa wa Kubadilisha Maisha Yako
Wewe unaweza na usiseme kuwa huwezi kufanya kitu fulani eti kwa sababu kwenu hakuna historia ya kufanya hicho kitu
Mungu ameamua kukutumia wewe kubadili historia ya Familia Yenu
Mungu amekuchagua wewe ili akutumie,akuinue,akupeleke mahali ambapo watu hawakutegemea kama wewe utafika ,ili wajue Mungu unaye muamini ni Muweza wa Yote
Jikubali kuwa unaweza,badilisha mtazamo wa kushindwa na weka mtazamo wa kushinda
Ipo nguvu ya Uzima ya kubadilisha Historia ya Maisha Yako
Usiwe muoga hakikisha hofu haipati nafasi katika maisha yako maana Mungu ana Mpango mzuri juu ya Maisha yako
Jiamini kwa kuwa Mungu yupo upande wako
Usiangalie nyuma na usiogope maneno ya watu ya kukukatisha tamaa
Songa mbele kwa kuwa KESHO YAKO NI NJEMA SANA NA INAPENDEZA
MUNGU AKUBARIKI

CONTACTS : WHATSAPP: +255756277095

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni