Breaking

Jumatano, 26 Agosti 2020

SOMO: YOTE YANAWEZEKANA KWA MUNGU



MWALIMU: MTUME DANIEL STANSLAUS
        Bwana Yesu asifiwe.Ninakukaribisha  tujifunze somo lenye kichwa cha habari kinachosema YOTE YANAWEZEKANA KWA MUNGU .
        Hakuna jambo lolote lile ambalo Mungu hawezi kulifanya katika maisha yako. Mungu ni muweza wa Yote na hajawahi kushindwa na  hawezi kushindwa kufanya lolote katika maisha yako.(Mwanzo 1:1Hapo mwanzo Mungu aliziumba mbingu na nchi)Maandiko yanaonyesha kuwa kila kitu kiliumbwa na Mungu,kwa hiyo Mungu anao uwezo wa kufanya jambo lolote lile na hakuna cha kumshinda.Aliweza kufanya uumbaji kwa kutumia Neno lake na kila alichosema kilitokea kwa hiyo  Neno la Mungu lina uwezo wa kufanya jambo lolote katika maisha yako hata kama hilo jambo unaliona kuwa lina ugumu kwake Mungu yote yanawezekana.Neno la Mungu haliangalii mazingira yanasemaje ili litimie bali linatimia bila kujali mazingira unayopitia (Mwanzo 1:3 Mungu akasema, Iwe nuru; ikawa nuru)
        Luka1:34-37Mariamu akamwambia malaika, Litakuwaje neno hili, maana sijui mume? Malaika akajibu akamwambia, Roho Mtakatifu atakujilia juu yako, na nguvu zake Aliye juu zitakufunika kama kivuli; kwa sababu hiyo hicho kitakachozaliwa kitaitwa kitakatifu, Mwana wa Mungu. Tena, tazama, jamaa yako Elisabeti naye amechukua mimba ya mtoto mwanamume katika uzee wake; na mwezi huu ni wa sita kwake yeye aliyeitwa tasa;kwa kuwa hakuna neno lisilowezekana kwa Mungu)Maandiko haya yanaonyesha kuwa Mariamu alikuwa na mtazamo wa kibanadamu na kuona kuwa kuchukua Mimba haiwezekani hadi amjue mume lakini kumbe Roho wa Mungu anauwezo wa kufanya jambo lolote.Mungu anachofanya ni kuhakikisha kuwa Neno lake linatimia bila kuangalia mazingira yanasemaje.Inawezekana una magonjwa ambayo madaktari wamesema kuwa hauwezi kupona,inawezekana watu wameshakata tamaa na maisha yako, inawezekana mateso unayopitia ni makubwa na unajiona kuwa unakaribia kufa lakini pia inawezekana jamii imekutenga au umeachwa kutokana na hali mbaya ya maisha unayopitia.Mungu wetu anaweza yote na anahangaikia maisha yako, Usikate tamaa kwa sababu Mungu anaishi na anayaona mateso unayopitia na atakusaidia na kukutoa kwenye mateso na kukuingiza kwenye maisha yenye raha na amani.Zaburi 113:7-9 Humwinua mnyonge kutoka mavumbini, Na kumpandisha maskini kutoka jaani.Amketishe pamoja na wakuu, Pamoja na wakuu wa watu wake. Huweka nyumbani mwanamke aliye tasa, Awe mama ya watoto mwenye furaha)Maandiko yanaonyesha kuwa ni tabia ya Mungu kumtoa mtu kutoka katika hali ya chini na kumuinua,tena amesema hata mwanamke akiwa tasa yeye Mungu anaweza kumpa watoto tena watoto wengi kwa hiyo usiogope yeye Mungu anaweza kufanya mambo yote.Mungu anachofanya ni kuhakikisha kuwa Neno lake au ahadi zake juu ya maisha yako zinatimia kwa hiyo atakupigania hadi pale ushindi wako utakapoupata,tena katika maandiko amesema kuwa yeye halali wala asinzii kwa ajili ya maisha yetu na kuhakikisha kuwa hakuna linashondikana katika maisha tunayoishi. (Isaya 62 : 1Kwa ajili ya Sayuni sitanyamaza, na kwa ajili ya Yerusalemu sitatulia, hata haki yake itakapotokea kama mwangaza, na wokovu wake kama taa iwakayo)
        Tunapaswa kujua kuwa Mungu ana njia zake ambazo hutumia ili kutupatia mahitaji yetu,kuna wakati njia za Mungu zinachukua mda  mrefu katika kutupatia majibu,na wakati mwingine njia za Mungu huwa zina majaribu Mengi na mazingira magumu ambapo inapelekea wanadamu kuona kuwa haiwezekani tena kufanikiwa.Njia za Mungu ni bora kuliko njia zote hata kama zinaumiza kwa sababu matokeo yake huwa ni mazuri sana yenye kumpa Mungu heshima na utukufu.Njia za Mungu sio za mwanadamu na mawazo ya Mungu sio sawa na ya mwanadamu.Isaya 55:8-9 Maana mawazo yangu si mawazo yenu, wala njia zenu si njia zangu; asema Bwana.Kwa maana kama vile mbingu zilivyo juu sana kuliko nchi, kadhalika njia zangu zi juu sana kuliko njia zenu, na mawazo yangu kuliko mawazo yenu.
        Ndugu yangu nataka nikuhakikishie kuwa Mungu wetu anaweza  mambo yote na hakuna jambo gumu kwake,ni wajibu wako kuendelea kuweka juhudi katika mambo yako lakini pia usiache kumuamini, kumtumaini na kumpa nafasi katika maisha yako ili uanze kuona mabo yote yakiwezekana katika maisha yako
Mungu akubariki sana
Kwa ushauri na maombezi unaweza kunipata kupitia namba hii  ambayo pia ina whatsapp 0756277095


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni